Monday, June 14, 2010

SARATANI YA TEZI LA KIBOFU

(PROSTATE CANCER)

“Gonjwa la wanaume tu! Madhara kwa familia nzima!”

Jee saratani ni gonjwa gani? Neno saratani ni jina la ugonjwa ambao hutokea wakati chembe chembe za uhai katika sehemu fulani ya mwili zinapoanza kukua bila kufuata utaratibu na mfumo wa mwili - zinaasi na kutengeneza vivimbe vidogo vidogo. Kwa kawaida chembe chembe za uhai mwilini huwa zinajigawa, zinapevuka na baadaye kufa kwa kufuata taratibu za mfumo wa mwili.
Lakini chembe chembe za uhai za saratani hazifuati mfumo huo. Badala ya kufa, zenyewe zinaishi mda mrefu kuliko chembe chembe za uhai za kawaida na wakati huo huo huendelea kutengeneza chembe chembe za uhai asi zingine na kutengeneza vivimbe vidogo vidogo, saratani.
Saratani ya tezi la kibofu ni gonjwa gani? Tezi la kibofu linapatikana katika mwili wa kiumbe mamalia dume tu (angalia mchoro - prostate). Chembe chembe za uhai katika katika tezi la kibofu zinapoanza kukua bila kufuata utaratibu na mfumo wa mwili - zinaasi na kutengeneza vivimbe vidogo vidogo, hapo mtu anakuwa amepata saratani ya tezi la kibofu. Zipo aina nyingi za saratani.
Zipo zinazowapata watoto tu, vijana, wanawake na wanaume. Saratani ya tezi la kibofu huwapata wanaume tu na hasa wenye umri wa takribani miaka 50 na kuendelea. Tokana na tafiti mbali mbali saratani hii imedhibitika kushika nafasi ya pili, ukiacha saratani ya mapafu kwa vifo vya wanaume wenye umri wa takribani miaka hamsini na kuendelea. Tafiti za Chama cha Saratani cha Marekani na cha Afrika Kusini vimebaini kuwa,“mwanaume mmoja kati ya sita atapata saratani ya tezi la kibofu katika uhai wake”.
Na kama wanaume mia moja wenye umri takribani miaka 50 na kuendelea wakigunduliwa kuwa na saratani za aina yoyote ile, asilimia ishirini na tano watakutwa na saratani ya tezi la kibofu. “Saratani hii haina mipaka ya kitabaka” asema Askofu Mkuu Desmond Tutu. A

skofu Mkuu Tutu, Mchungaji Kanoni Dk. Emmanuel Kandusi na Rais Mstaafu wa Afrika ya Kusini Mzee Nelson Mandela ni baadhi ya wahanga wa gonjwa hili ambao bila ya kujinyanyapaa na wala hofu ya kunyanyapaliwa, wamevunja ukimya na kuwa wawazi katika jamii. Pamoja na yote hayo, ifahamike bayana, saratani ya tezi la kibofu ikigundulika mapema inatibika kwa urahisi zaidi.

Hali hatarishi: Kuna hali hatarishi nyingi zinazochangia mwanamume kupata saratani ya tezi la kibofu. Kati ya hizo nyingi hapa ntazitaja tano tu. Kwanza ni umri: Nafasi ya kupata saratani ya tezi la kibofu inaongezeka sana hasa ukifikia umri wa takribani miaka 50 na kuendelea. Nasaba: kama katika ukoo kuna historia ya ugonjwa wa saratani ya tezi la kibofu suala na nasaba linachangia kumweka mwanamume kuwa hatarini kupata saratani ya tezi la kibofu kwa misingi ya nasaba (genetic).

Lishe: wanaume wanaopenda kula nyama yenye mafuta mengi na aina ya maziwa yenye mafuta mengi (high-fat diet) wako katika hatari kubwa ya kupata saratani ya tezi la kibofu; Mazoezi: Wanaume wasiopenda kufanya mazoezi na Unene (obesity). Vitamini D: Upungufu wa Vitamini D.

Dalili za saratani ya tezi la kibofu: .Swali linakuja: Jee mwanamume ataziona dalili zipi zinazoashiria ana saratani ya tezi la kibofu? Zipo dalili nyingi na hapa naziitaja baadhi tu:

Udhaifu katika kujisaidia haja ndogo na unapotoka unakatizwakatizwa;
Kushindwa kukojoa na kushindwa kuanza pata haja ndogo;
Unapohisi haja ndogo unapata shida kuzuia haja ndogo isijitokee yenyewe;
Haja ya kutaka kupata haja ndogo kila wakati hasa nyakati za usiku; hata kukojoa kitandani;
Mkojo kujitokea wenyewe;
Maumivu au kuhisi mwasho wakati wa haja ndogo;
Mbabaa kusimama kwa shida;
Maumivu wakati unapotoa manii wakati wa kujamiana;
Damu damu katika mkojo na katika manii;
Maumivu kiunoni au pajani hasa mguu wa kushoto.
Kukosa hamu ya kula na kupungua uzito / kukonda.
Pamoja na kuorodhesha dalili hizo napenda msomaji ujue kwamba mwanaume anapoanza kuziona na kuzihisi kati ya dalili hizo, basi ajue chembe chembe za uhai asi katika tezi la kibofu chake zina umri wa takribani miaka minane na kuendelea.
Uchunguzi: Kwa kuzipitia dalili hizi, imegundulika kuwa wanaume wengi wakiziona na kuzihisi huwa na soni kwenda kumwona daktari kwa uchunguzi. Wengi huzihusisha na magonjwa ya zinaa au kuzihusiza na dhana potofu za kishirikina kwamba mtu kalogwa. Wapo wanaokwenda mbali zaidi hata kuuita ni ugonjwa wa mabasha na wengine kuurahisisha kama ugonjwa wa utu uzima kana kwamba saratani ya tezi la kibofu ni haki yake kuugua mtu mwenye umri wa takribani miaka hamsini na kuendelea.

Mambo kama hayo huleteleza wazee kujinyanyapaa na kujikuta wengine wakijitibu chochoroni au kwa waganga wababaishaji mpaka pale wanapokuwa hoi bin taabani, mambo yamekuwa mabaya ndipo wanapopelekwa hospitalini.

Hapa tunatoa wito kwa wazee kuweka kipaumbele tabia ya uchunguzi wa afya kwa ujumla na ukifikia umri wa takribani miaka 50 na kuendelea uchunguzi huo ujumuishe uchunguzi wa tezi la kibofu angalau mara moja kwa mwaka. Kuwahi kugundua saratani hii kabla hata ya kuziona dalili hizo ni faida kubwa kwa mwathilika kwani saratani hii ikigundulika mapema ni rahisi kutibika.

Matibabu: Ifahamike kuwa katika zama hizi matibabu ya saratani yapo na pia ijulikane kuwa kadri saratani ikigundulika mapema tiba yake inakuwa nyepesi zaidi. Zama hizi kuna tiba nyingi hapa nazitaja nne mahsusi. Kuna tiba ya uangalizi (active surveillance), upasuaji (prostatectomy), mionzi (radiotherapy) homoni (hormone therapy) na kemikali (chemotherapy). . Mwathilika ukigundulika una saratani ya tezi la kibofu unashauriwa ushauriane na daktani wako na kuamua tiba itakayokufaa.

Tanzania 50 Plus Campaign: Kampaini hii imeanzishwa na Centre for Human Rights Promotion – CHRP Dodoma (Kituo cha Kukuza Haki za Binadamu). Lengo kuu la kamapeini hii ni kupunguza maumivu na vifo vinavyotokana na saratani ya tezi la kibofu. Kampeini inatarajia kufikia lengo lake kwa kutekeleza shughuli zifuatazo:

Uhamasishaji: Kuelimisha na kusambaza habari juu ya ugonjwa huu. Kuwatia moyo wanaume wote wenye umri takribani miaka 50 na kuendelea kwenda hospitali kupata huduma za uchunguzi wa tezi la kibofu na watakaobainika kuwa na matatizo kupata matibabu;
Mradi darasa: Kampeini imechagua Wilaya ya Kongwa kuwa mradi darasa. Katika wilaya hii tutafanya utafiti jamii kubaini idadi ya wazee na kuwafanyia uchunguzi wa tezi la kibofu. Watakaopatikana wana tatizo la aina yoyote katika tezi la kibofu, kwa kushirikiana na ndugu zao watapatiwa matibabu;
Uwezeshaji: Tutahamasisha Wizara ya Afya na Utawi wa Jamii, wafadhili wa nje na ndani, jamii kwa ujumla ili vifaa hivi vya kufanyia uchunguzi na vya tiba ya saratani ya tezi la kibofu vinapatikana na kuwekwa katika hospitali na vituo vyote vya afya nchini. Vifaa vinavyotakiwa ni “Semi Automated Eliza Machine Stat Fax 303 with Washer”158 (bei Tshs. 7.5 ml kila kimoja) and na paketi 1,580 za vitenganishi “Prostate Specific Antigen Reagents” (bei Tshs. 220,000 kila paketi);
Vikundi vya Misaada: Tutafungua vikundi vya misaada kwa wahanga, wenzi na familia. Katika vikundi hivi ushauri nasaha utatolewa na pia kuwasaidia waathilika wapya;
Haki za Binadamu: Afya ni haki ya kila binadamu. Kampeini itazingatia maudhui hii na kuwa ndio nguzo ya kampeini nzima.

KAMPAEINI INAKAZIA WITO KWA MSISITIZO:

Kwa wanaume wote wenye umri takribani miaka 50 na kuendelea, tafadhali mwone daktari wako kwa uchunguzi wa afya ukijumuuisha uchunguzi wa tezi la kibofu;



Pia wito kwa madaktari wote, mnapopata wagonjwa wenye umri takribani miaka 50 na kuendelea washaurini pamoja na matibabu mengine, wafanyiwe uchunguzi wa tezi la kibofu.



TAFADHALI TAMBUA:

“Saratani ya tezi la kibofu ikigundulika mapema ni rahisi kutibika”

Kwa wasomaji wote:

OKOA MAISHA

UNGA MKONO KAMPEINI HII:

Wasiliana na:

MRATIBU WA KAMPEINI

Tanzania 50 Plus Campaign

Prostate Cancer: Literacy and Support Initiative

P. O. Box 1854

DAR ES SALAAM – TANZANIA

Simu: +255 754 402033 begin_of_the_skype_highlighting +255 754 402033 end_of_the_skype_highlighting Barua pepe: tanzania50plus@yahoo.com

No comments:

Post a Comment