Sunday, May 30, 2010

Kaberuka achaguliwa tena kuwa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)


Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika leo tarehe 27 mwezi mei hapa Abidjan imemchagua tena Bw.Donald Kaberuka kuwa Rais wa Benki hiyo kwa kipindi cha pili. Bw. Kaberuka alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa Rais wa Benki hiyo mwaka 2005.Kuchaguliwa kwake kwa kipindi cha pili kumetokana na mafanikio makubwa ambayo ameyaleta katika benki hiyo na kuleta maendeleo katika taasisi hiyo muhimu ya kifedha na kwa bara la Afrika. Hii ilibainika kutoka kwa Magavana waliotaka Rais huyo kuendelea na wadhifa wake.Katika kukubali kuthibitishwa kwake katika cheo hicho.
Bw Kaberuka aliwashukuru Magavana hao kwa kuwa na imani na uongozi wake katika benki. “Nina farijika sana kuona kuwa ninyi Magavana mna imani kubwa na mimi hadi kunichagua tena ili niweze kuiongoza taasisi hii muhimu, kwa kweli nina shukuru sana”,alisema." Ningependa kutoa shukrani zangu za pekee kwa uongozi na wafanyakazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika kwani wao ndio wamenifikisha hapa kwani mimi ni Rubani tu. Alisema Kaberuka baada ya kuthibitishwa katika nafasi hiyo.“Nilichaguliwa kwa mara ya kwanza miaka mitano iliyopita.
Benki imeongezeka mara mbili .
Lakini katika kipindi cha miaka mitano ijayo, tutajikusanya na kuiweka Afrika katika kiwango cha juu kimataifa",alieleza."Tutajitahidi kuhakikisha kuwa tunafikia mategemeo ya watu wa Afrika. Tutafanya kazi ilitufikie lile lengo la kuwa na bara moja linaloshirikiana kwa kila kitu, tutapambana na mabadiliko ya hali ya hewa na kuhakikisha kuwa tunakuwa na chakula cha kutosha, alisema.Kikosi cha Benki ya Maendeleo ya Afrika kimekuwa na maendeleo makubwa katika shughuli zake za ndani na uongozi, vilevile imelenga zaidi uwajibikaji katika kuleta maendeleo Afrika hasa katika kukuza sekta binafsi, kufadhili miradi inayoshughulikia miundo mbinu, na kusisitiza kuwepo biashara ya pamoja katika kukuza uchumi wa bara la Afrika.Katika ripoti iliyotoka hivi karibuni inayohusu muonekano wa Uchumi katika Bara la Afrika inasema kuwa, ifikapo mwaka 2011 uchumi utakuwa kwa asilimia 5.2 tofauti na kiwango cha sasa cha asilimia 4.5 kwa mwaka 2010.Kwa sababu ya kuongezeka kwa mahitaji ya Benki ya maendeleo ya Afrika Benki imekuwa na uhaba wa fedha uliosababishwa na mtikisiko wa uchumi. Kwa sababu hiyo basi Magavana pia wametoa uhalalisho wa kuongeza mtaji kwa taasisi zake kwa asilimia 200% hii itasaidia kuendesha miradi na programu ambazo nchi wanachama imezipanga.Chini ya uongozi wa Bw.
Kaberuka Benki imejitahidi kuhakikisha kuwa kunakuwa na mawasiliano ya karibu kati ya nchi zilizoko kwenye ukanda mmoja na sekta binafsi. Aidha benki imefanikiwa kuwa na ofisi katika kila nchi barani Afrika.Magavana waliainisha.
Bw. Kaberuka, ambaye ni Rais wa saba wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, aliapishwa tarehe 1 mwezi septemba mwaka 2005 kwa mara ya kwanza huko Tunisia.Kabla ya kujiunga na Benki, Bw. Kaberuka alikuwa Waziri wa fedha na mipango ya Uchumi wa Rwanda kuanzia mwaka 1997 mpaka 2005, na alitambulika kama Mkuu aliyejenga upya nchi ya Randa ambayo ilikuwa na vita na aliweza kuijenga nchi hiyo kwa kuweka programu nzuri zilizoleta mabadiliko ya uchumi.Alianzisha na kuendeleza maboresho katika uongozi na uchumi mkuu katika mambo ya fedha, mambo ya mabenki, bajeti, miundo muhimu ya nchi ikiwa ni pamoja na benki kuu ya nchi iliyo huru.
Na matokeo ya maboresho hayo ni kukua kwa uchumi wa Rwanda ulio imara na kuiwezesha nchi hiyo kufaidika kwa kufutiwa madeni yake mwezi Aprili mwaka 2005.
Bw. Kaberuka anauzoefu wa zaidi ya miaka 12 katika mambo ya Benki, katika mambo ya fedha na biashara, katika mambo ya biashara ya vitu kimataifa na katika maendeleo ya sekta kabla yakujiunga na serikali.
Akiwa Waziri wa Fedha na mipango kiuchumi, Rais huyu wa Benki ya maendeleo ya Afrika alitumika kama Gavana wa Benki ya Dunia kwa Rwanda, vilevile katika shirika la fedha la kimataifa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.Alisoma Tanzania hadi kidato cha sita na kupata shahada ya kwanza katika chuo kikuu cha Dar es salaam.
Vilevile alisoma Uingereza ambapo alipata shahada ya uzamili katika filosofia ya Uchumi na uzamifu katika filosofia ya Uchumi huko chuo kikuu cha Glasgow - Scotland.
Bw. Kaberuka anazungumza vizuri sana Kiingereza, Kifaransa na Kiswahili.
Ingiahedi MdumaMsemaji Mkuu- Wizara ya fedha na UchumiAbidjan.

No comments:

Post a Comment