Wednesday, February 16, 2011

Sitta, Mwanjelwa nao wajitosa Tamasha la Pasaka

WAZIRI wa Afrika Mashariki na Mbunge wa Urambo kupitia CCM, Samuel Sitta amempongeza Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya tamasha la Pasaka, Alex Msama kwamba fedha zake zinazopatikana zinafanyiwa kazi zilizokusudiwa.

Tamasha la Pasaka la mwaka huu litakalofanyika Aprili 24 lengo lake kubwa kwa mujibu wa Alex Msama ni kwa ajili ya kuwasomesha watoto yatima na kuwasaidia mitaji ya biashara wanawake wajane.
Sita amesema kwamba jitihada zinazofanywa na Alex Msama ni mfano wa kuigwa kwa vijana wengi hapa nchini, kwani anaisaidia jamii kwa mapenzi kutoka moyoni.
“Kwa kweli kama wangejitokeza vijana wengine kama Msama naamini kabisa jamii yetu ingekuwa inapata misaada mingi, kwani jitihada anazozifanya ni za kumpongeza.”
Alisema ameshuhudia walemavu wakinunuliwa baiskeli, watoto yatima wakisomeshwa na wajane kusaidiwa mitaji ya biashara kupitia fedha alizozipata Msama kupitia matamasha pa Pasaka yaliyopoita.
Aliongeza kusema kwamba kwa kiasi kikubwa tamasha hilo pia litasaidia kupunguza tatizo la ajira kwa vijana, kwani wengi hivi sasa wameamua kujikita katika muziki wa injili kwa ajili ya kumuimbia Mungu na kujipatia kipato.
“Unapokuwa na watu wenye uzalendo kama Msama Promotions kwa hakika kabisa vijana wengi watajitokeza na watahamasika kujiingiza katika muziki huu, kwani watakuwa na uhakika wa kujipatia kipato,” alisema Sitta.
Wakati huo huo Mbunge wa viti maalumu kupitia chama cha Mapinduzi mkoani Mbeya, Mary Mwanjela amejitokeza kumpongeza Msama kwa kuandaa Tamasha hilo.
Pia hivi karibuni aliyekuwa Waziri Bunge, Sera na Uratibu katika awamu ya kwanza ya rais Jakaya Kikwete, Phillip Marmo alilisifia tamasha la Pasaka kwa kusema kwamba malengo yake ni mazuri kwani linasaidia jamii.

No comments:

Post a Comment